Thursday, September 25, 2014

VITA DHIDI YA HATIMA YA MAISHA YAKO

Mwl. ERASTO KIBIKI
Hatima ni lile kusudi la milele ambalo mwanadamu ameumbiwa alitimize akiwa hapa duniani, kama tunavyosoma katika biblia kuwa “Daudi baada ya kulitimiza kusudi la Mungu wake akalala na baba zake

Hatima {Destiny}  ni ule wito unaokufanya uishi hapa duniani na baada ya kuukamilisha unarudi mbinguni kwa Mungu wako.

Hatima ya maisha ni kitu muhimu sana kukijua kabla ya kuvijua vitu vyote, maana hatima ni zile ndoto za maisha yako ambazo kwa hizo unakula, unakunywa, unapata makazi na malazi. Kwa hatima yako unapata pesa inayokuwezesha kuishi vizuri na kuwa msaada katika jamii inayokuzunguka.

Wednesday, September 24, 2014

UMUHIMU WA TOBA KWA KANISA LA SASA

SEHEMU YA KWANZA

Mwl: Elia Agrey

MAANA YA TOBA

Bwana YESU apewe sifa; ninayo kila sababu ya kumshukuru Mungu anayetupa uzima huu tulio nao kwa Neema, yaani bure bila kulipia chochote. hivyo basi ni maombi yangu kwa Mungu kukusaidia kuelewa somo hili ambalo ni muhimu sana kwa kanisa la sasa kuliko unavyoweza kufikiri na kuyaweka katika matendo yale utakayojifunza. Fuatana na mimi katika somo hili ili uwe sehemu ya mabadiliko ambayo Mungu anataka kuyafanya katika Kanisa ambalo ni mimi pamoja na wewe.

Unaposoma Biblia katika kitabu kile cha Matendo ya Mitume 3:19 Biblia inasema ‘…Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake…”

Katika tafsiri ya the living Bible  Biblia inasema “…Now change your mind and attitude to God and turn to Him so that He can cleanse away your sins and send you wonderful times of refreshment from the presence of the Lord…”

Unaposoma katika tafsiri hizi zote mbili za Biblia unapata maana nzuri ya TOBA ambayo ni kurejea na kuacha kufanya kitu ambacho ulikuwa unakifanya na Mungu hataki na hapendi wewe ukifanye.Biblia ya kiingeleza imesema “ Change your mind and attitude ” kwa iyo unaona kuwa TOBA ni kubadilisha mtazamo wako na mawazo kumulelekea Mungu na kuacha kuelekea dhambi. Kinachomfanya Mungu akusamehe dhambi zako ni kule kubadilisha mtazamo wako na mawazo yako yasiyoendana na Mungu. Kwa kifupi tunaweza kusema kuwa TOBA ni kugeuka kutoka katika jambo ambalo Mungu amelikataza na kutenda lile ambalo Mungu ameliagiza kufanya

Si suala tu la kugeuka lakini ni kuenda mbali na yale mambo ambayo Mungu amekuambia kwa Neno lake ya kuwa usifanye

CHANZO CHA TOBA
Toba imekuja kwa sababu ya dhambi kusingekua na Toba kama hakuna dhambi na Bilbia inatuambia dhambi ni uasi (1 Yohana 3:4) na uasi ni kuenda kinyume na maagizo ya Mungu. Kwa iyo kilichosababisha dhambi ije na kutawala duniani ni uasi ambao mwanadamu aliufanya dhidi ya Mungu.
Dhambi iliingia duniani kwa njia ya KUSIKIA, KUAMINI na KUTII uongo wa shetani.Adamu ambaye ni mwanadamu wa kwanza na mtangulizi wetu kama baba yetu wa kwanza ALISIKIA, ALIAMINI, na AKATII uongo wa shetani na ivyo akaruhusu dhambi kuingia ulimwenguni. Warumi 5:12

“…Kwa hiyo, kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi…”

Aliyesikia ni Adamu aliyeamini ni Adamu na aliyetii uongo wa shetani ni Adamu lakini dhambi ikatufikia watu wote kwa kuwa tu uzao wa Adamu wa kwanza. Unaposikia unapoamini na unapotii kile ambacho shetani kwa kupitia kitu chochote amekushawishi kukifanya unatenda dhambi juu ya Mungu na ndipo TOBA inahitajika katika maisha yako.Mungu hapendi wanadamu waishi chini ya mfumo wa dhambi na ndio maana alianzisha mfumo mpya kwa mwanadamu wa kumrudia yeye baada ya kukosea na mfumo huo ni kwa njia ya TOBA. Alimfanya mwanawe Yesu Kristo asiye na dhambi kuwa dhambi ili kwa kupitia yeye aliye mkamilifu wanadamu wapate ondoleoo la dhambi milele (1Korintho 5:21)

Kwa hiyo toba iliingia kwa njia ya KUSIKIA, KUAMINI na KUTII kile ambacho Mungu amesema.Yesu ambaye ni Adamu wa mwisho (1 Korintho 15:45) ALISIKIA, AKAAMINI na KUTII maagizo ya Mungu na ivyo kuuondoa ule uasi ambao Adamu wa kwanza aliufanya. hivyo kwako wewe ambaye ni sehemu ya Kanisa la Mungu unapata TOBA kwa KUSIKIA, KUAMINI na KUTII maagizo ya Mungu katika maisha yako

KWA NINI TUNAHITAJI TOBA
Kuna mambo mengi ambayo hayaendi sawa katika kanisa la Mungu na ili yaende sawa tunamuhitaji Mungu aingilie kati kwa njia ya TOBA.Kama Kanisa la Mungu nikimaanisha mtu aliye mwamini YESU KRISTO likikosea au akikosea mambo mengi katika maisha yake na ya watu wengine wanaounganishwa naye hayawezi kuenda sawa hii ikiwa na maana kuanzia katika ngazi ya chini kabisa katika familia na hata ngazi ya juu zaidi katika taifa hayawezi kuenda sawa maana kuna makosa yaliyofanywa na hayajatubiwa

Ukisoma katika kitabu kile cha Warumi 3:23 utaelewa vizuri kile ninachosema Biblia inasema “… kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu;…”

Unapofanya dhambi yoyote katika maisha yako utukufu na uwepo wa Mungu katika maisha yako unapungua na hivyo kufanya kiwango cha Mungu kushugulika na maisha yako kupungua siku hadi siku. Kwa hiyo wewe kama sehemu ya kanisa unapokuwa umefanya dhambi na haujatubu UTUKUFU na UWEPO wa Mungu uliokuwa katika maisha yako unapungua na hivyo kufanya nguvu na uwepo wa Mungu uliokuwa unashugulika na maisha yako na wote wanaounganishwa na wewe kupungua katika maisha yako na unapozidi kupungua ndipo uwepo wa shetani na nguvu za shetani zinapozidi kuyatawala maisha yako na maisha ya wote uliokuwa unaunganishwa nao kama sehemu ya kanisa


Mahusiano uliyokuwa nayo na Mungu kama Kanisa yanaharibika kabisa kwa sababu ya dhambi,Mungu alikuwa rafiki yako lakini anakua adui yako huoni tena sababu ya kuwa karibu na Mungu unafanya mambo yasiyompendeza Mungu kabisa.Na hiki ndicho kilichotokea hata kwa Adamu baada ya kumuasi Mungu akaona ajifiche mbali na uso wa Mungu akijua Mungu hamuoni. Mungu anachohitaji kutoka kwako baada ya kukosea ni wewe kuomba TOBA kwake na wala sio kujificha mbali naye na kuendelea kufanya yaliyo maovu zaidi. Sio suala la kuendelea mbele kana kwamba hujui kosa ulilolifanya na hujali kwamba umefanya bali ni suala la Kurudi na kuzingatia kisha kuungama dhambi zako ulizozifanya 
Ufunuo 2:5”… Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu…” 

 Suluhisho ni kukumbuka kosa kisha kutubu na kubadilisha muelekeo uliokuwa unaenda nao.Anaposema kumbuka ni wapi ulikoanguka ukatubu hana maana kwamba uikumbuke dhambi namna ulivyofanya la hasha ana maana yakumbuke mazingira yaliyokupelekea wewe ukafanya dhambi kisha epukana na hayo mazingra na ubadilishe muelekeo wako katika mazingira yaliyokufanya umkosee Mungu. Suala la kuanguka lipo lakini Biblia inatufundisha kitu kimoja muhimu sana kuwa ukianguka USIKAE hapo hapo na kukubaliana na hali iyo bali INUKA na UTUBU. Usikae hapo hapo wala usiinuke na kuendelea mbele KANA KWAMBA hakujatokea kitu bali INUKA na UTUBU

Monday, September 22, 2014

MWITE YESU WAKATI WOTE

Katika maisha usiogope kumwita Yesu, mwambie akuokoe ili usizame katika tamaa, anasa na udanganyifu wa mali za hapa duniani hata ukaipoteza nafsi yako ya thamani. nasisitiza tena, jiponye nafsi yako nawe ukaishi milele na Bwana katika ile mbingu mpya na nchi mpya aliyotuandalia; maana alisema 

"Naenda kwa Baba kuwaandalia makao, ili nilipo Mimi nanyi muwepo, na tazama Maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake, Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao" Ufunuo 21:1-9

Makao yamesha andaliwa na yanaendelea kuandaliwa, tujiandae maana wakati tusioudhani parapanda italia, wafu watafufuliwa na sisi sote tutamlaki Bwana mawinguni pamoja na mwaliko wa watakatifu, HAKIKIKISHA UNAKUWA MIONGONI MWA WATEULE kwa kuutunza utakatifu na kuokoka hali ungali hapa duniani.

PICHA

Mwl. Elia Agrey akiwa katika ibada kabla ya huduma mkoani mbeya


















Mwimbaji Cornel Mwangolombe akiwa katika huduma mkoani mbeya




Wednesday, September 17, 2014

WOKOVU

Inawezekana neno hili wokovu au kuokoka sio geni masikioni mwako umelisikia mara nyingi na una maana nyingi kuhusu wokovu. Lakini embu tuangalie Biblia inasemaje kuhusu wokovu

Warumi 10:9-10 Biblia inasema “… Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu…”

hivyo kwa tafsiri iliyo nyepesi WOKOVU ni kumkubali Yesu Kristo kuwa ni Bwana
Na Mwokozi wa maisha yako. Unamkubali moyoni mwako na kusema kwa kinywa chako kile ulichokiamini na kukikubali moyoni mwako.

Kwa hiyo wokovu au kuokoka ni KUAMINI moyoni na KUKIRI mdomoni ya kuwa YESU KRISTO ni Mwana wa Mungu na yakuwa Mungu alimtuma ili aje kuwaokoa wanadamu ambao ni mimi na wewe, kila anaye amini ya kwamba YESU KRISTO alitumwa na Mungu aje duniani ANAOKOKA

Yohana 3:16 “… Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele…”

Kilichomfanya Mungu amtume mwanawe tena wa pekee aje duniani kuutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu waliokuwa katika dhambi ni UPENDO wake juu ya wanadamu. Aliwapenda wanadamu kwanza ndipo akamtuma YESU KRISTO aje duniani kwa ajili yetu.
Kila mtu anaye mwamini YESU KRISTO anafanyika kuwa mwana wa Mungu na kuingia katika ufalme wa Mungu ulio wa milele.

Mungu hakutamani na wala hatamani kuona wanadamu wanapotea nje na Kweli yake, ndio maana Yesu Kristo alikuja ili atuonyeshe Njia itupasayo kuiendea ili tusizidi kupotea

Yohana 14:6 “…Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi…”

Mungu anataka wanadamu wote tuijue Njia yakumfikia yeye na Njia hiyo ni YESU pekee hakuna NJIA nyingine ya kumfikia Mungu isipokuwa kwa kupitia YESU KRISTO pekee, kwa sababu hiyo ukimwamini YESU KRISTO kuwa Bwana na Mwokozi na Kiongozi wa maisha yako UTAOKOKA na kuupokea uzima wa milele ndani yako na hatimaye utamfikia Mungu na kumuona Mungu na kuishi naye milele na milele
Mathayo 10:32-33
“…Basi kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni.Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni…”

Unayo nafasi sasa ya kumpa Yesu maisha yako UKIAMINI kwa moyo wako na KUKIRI kwa kinywa chako kuwa YESU KRISTO ni BWANA na Mwokozi na Jina lako litaandikwa Mbinguni; Yesu ameahidi Kukukiri Mbele za MUNGU mbinguni lakini pia kama ukimkana huku duniani kwa kutoamini naye pia atakukana mbele za Baba yake aliye mbinguni.

Ikiwa hujaokoka na ungependa kuokoka sema nami sala hii kwa sauti hapo ulipo
Nakushukuru Mwenyezi Mungu kwa upendo wako kwangu, nakushukuru kwa kumtuma mwanao YESU KRISTO aje kufa msalabani kwa ajili ya dhambi zangu, naomba unisamehe dhambi zangu zote nilizokukosea katika maisha yangu, futa jina langu kwenye kitabu cha mauti na andika jina langu kwenye kitabu cha UZIMA, kuanzia leo mimi ni mali yako. namkataa shetani na kazi zake zote, unipe ROHO wako akae nami siku zote za maisha yangu; katika Jina la YESU KRISTO Amen.

Ikiwa umesema sala hiyo basi tayari umeokoka na Yesu Kristo yuko ndani yako kwa imani
Mungu azidi kuwa nawe akikufundisha na kukutunza katika Jina la YESU Amen.

tafuta kanisa lililo karibu nawe linaloamini na kufundisha habari za wokovu na ondoleo la dhambi za wanadamu ukajiunge nao ili uendelee kuukulia wokovu wako.

Tuesday, September 9, 2014

VIDEO



AUDIO

MAFUNDISHO

Mwl Erasto Kibiki
NAMNA YA KUFANIKIWA KATIKA ELIMU

Sehemu ya kwanza
Kila mtu ana namna na mfumo wake wa kusoma, lakini namna unavyosoma sasa inaweza kuwa haikufai zaidi katika mafanikio yako kielimu. Utajuaje? Ni rahisi tu! Kama matokeo yako katika mitihani mbalimbali hayalingani na matarajio ya ufaulu wako uliyojiwekea, basi inatakiwa ubadilishe namna unavyosoma.

Dunia ya leo ipo katika mabadiliko makubwa sana yanayotokana na kuongezeka kwa maarifa, na kuendelea kwa sayansi na teknolojia kama ilivyotabiriwa kuwa “Hata wakati wa mwisho wengi wataenda mbio huko na huko na maarifa yataongezeka” (Danieli 12:4c) hali inayopelekea elimu kuhitajika sana na kuwa na thamani zaidi ukilinganisha na kabla ya mabadiliko haya kutokea.

Katika kitabu hiki, nimeelezea kwa sehemu dhana nzima ya elimu, utofauti wake na masomo ya darasani, mambo muhimu ya kufanya ili kila mtu afanikiwe katika elimu yake na aina nyingine za elimu ambazo upatikanaji wake hutofautiana kulingana na mahitaji ya kila mtu.

TAFSIRI YA ELIMU
Elimu ni ujuzi aupatao mtu kwa njia yoyote unaomsaidia kuishi hapa duniani kwa maisha ya sasa na yajayo; ujuzi huu waweza kupatikana kwa njia ya asili au kwa njia isiyo ya asili. Elimu ni ufunguo wa ukombozi na chombo muhimu cha kupunguza matatizo ya jamii na uchumi, kwani elimu ni tendo au uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa kimaumbile wa mtu binafsi.

Katika dhana ya kiufundi, elimu ni njia ambayo hutumiwa kimaksudi na jamii kupitisha maarifa, ujuzi na maadili kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Maana mbalimbali za elimu zina dhana kuu moja ambayo ni kupitisha maarifa katika vizazi tofauti tofauti.

Upana wa elimu huthibitisha kuwa kiwango cha maarifa hapa duniani kimeongezeka kama ilivyotabiriwa katika maandiko matakatifu kuwa “…hata wakati wa mwisho, wengi wataenda mbio huko na huko na maarifa yataongezeka”. (Daniel 12:4) zaidi ya yote “ Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; mshike maana yeye ni uzima wako” (Mithali 4:13).

Ujuzi wowote ulionao ndiyo elimu yenyewe, hivyo Maisha bila elimu ni sawa na bure, ndio maana tunatakiwa kuwa na ujuzi wowote  utakaotusaidia kuishi vizuri hapa duniani, hapa mtunzi wa mithali hii ameifananisha elimu na kiumbe hai, hata akasema “mshike maana yeye ni uzima wako” hivyo kiwango cha maisha utakayoishi hapa duniani kinategemeana na aina ya ujuzi ulionao na jinsi unavyoutumia.

Mafanikio ya kielimu yana gharama zake zinazotakiwa kulipwa na mhusika kwa wakati na majira sahihi, uwe na uhakika kuwa ujuzi huu utakusaidia sana katika shule yako na maisha kwa ujumla.

AINA ZA ELIMU
Kwa kawaida elimu ni pana sana, kama tunavyojua kuwa ujuzi wowote alionao mtu huitwa elimu kama elimu ya biashara, elimu ya ufundi, elimu ya viumbe hai, elimu ya maisha na kadharika. Elimu hufananishwa na ghara lililojaa aina mbalimbali za vyakula na kama mafuta ghafi ambayo yakichujwa hutoa aina mbalimbali za mafuta kama Diesel, Petrol na mafuta ya taa.

Masomo ya darasani ni sehemu ya elimu na wala sio elimu yenyewe, ni kama kitendea kazi ndani ya elimu na zipo aina kuu mbili za elimu ambazo ni Elimu rasmi na Elimu isiyo rasmi na ndani yake kuna aina ndogo ndogo za elimu zinazounda aina kuu mbili za elimu kama zilivyotajwa hapo juu.

1.      ELIMU RASMI - [ formal education]
Hii ni aina ya elimu tunayoipata darasani moja kwa moja kwa kutumia masomo maalum yanayofundishwa na walimu wetu, kwa kawaida aina hii ya elimu imewekwa na kupangwa kwa madaraja mbalimbali kuanzia ngazi ya shule ya msingi mpaka chuo kikuu; madaraja makuu ni elimu ya msingi, elimu ya sekondari na elimu ya juu {chuo kikuu}.

Pia inahusisha masomo ya taaruma kwa ujumla na aina mbalimbali za mipango {program} maalum kwa wanafunzi wanaosoma muda wote {full time students}, kwa wale wanaosomea elimu ya ufundi na utaalam ambao hupelekea kutunukiwa vyeti. Elimu hii hufuata mtaala maalum unaoisha kwa kipindi maalum wenye himizo maalum katika mitihani na kutunukiwa vyeti.

Jamii huitambua sana elimu hii na mtu ambaye hajaenda shule hudharauliwa na kuonekana kama hajaelimika hata kama ana ujuzi unaomfanya aishi vizuri kitu ambacho si kweli.

NGAZI ZA ELIMU RASMI
Elimu rasmi ina ngazi kuu mbili ambazo ni elimu ya kawaida na elimu ya juu. Elimu ya kawaida ina vipengere vifuatavyo. Elimu ya msingi, Elimu ya sekondari (O-LEVEL & A-LEVEL), ngazi ya cheti (Certificate) na ngazi ya Diploma. Kwa kawaida mtu anayefauru katika ngazi hizi hupata fursa ya kusoma elimu ya juu.

Elimu ya juu ina ngazi zifuatazo, ngazi ya shahada ya kwanza (Degree), ngazi ya uzamili –shahada ya pili (Masters), ngazi ya uzamivu au shahada ya tatu (Doctorate) na hatimaye kuwa mtaalam maalum yaani uprofesa (Profession).

2.      ELIMU ISIYO RASMI (Informal education)

Huu ni mchakato wa kuyapata maarifa au ujuzi na mbinu mbalimbali kutokana na mitazamo tofauti tofauti inayopatikana siku hadi siku pale ambapo mtu anashabiliana na mazingira yanayomzunguka.

Mchakato huu hauna mpangilio maalum, wala mwongozo rasmi na haujawa na lengo maalum; watu huipata elimu hii kwa kuchunguza mambo na kuhusika moja kwa moja pale wanapohusishwa kufanya kazi au jambo Fulani la kijamii katika mfumo wa maisha ya kila siku. Kwa kupitia mshabiliano (interaction) ndani ya familia, wakati wa matembezi, safarini, masokoni, maktaba, kwa njia ya vyombo vya habari na maeneo yoyote yenye watu.

Ndani ya tamaduni mbalimbali zisizojua kusoma wala kuandika, elimu hii huchukua sehemu kubwa sana ya kuelimisha jamii na kuendeleza maarifa kwa kizazi kimoja na kingine. Hivyo umuhimu wa elimu hii ni katika kumwezesha mtu kukabiliana na changamoto za mara kwa mara na kukidhi mahitaji yake. Na elimu za aina zote ni muhimu kwani hutegemeana na zote hupitisha maarifa kizazi hadi kizazi.

UMUHIMU WA KUWA NA BIDII KATIKA ELIMU

Bidii inahitajika katika kufanikisha jambo lolote, na kujibidiisha katika kuipata elimu hutoa nafasi kubwa ya kufikia viwango vikubwa vya mafanikio maishani, ni vyema sana kufanya kazi kwa bidii ili ule chakula chako mwenyewe na unywe maji ya birika lako mwenyewe.

Zaidi sana “Yafahamu sana haya nisemayo, kwa maana Bwana atakupa akili katika mambo yote” (2Timotheo 2:7) hii ikiwa ni pamoja na masomo ya darasani. Kwa wanafunzi walioko sekondari ambao ni O-level na A-level, ni muhimu kusoma sana ili kufikia kiwango cha elimu ya juu (Chuo kikuu) ambayo huongeza kwa kiasi kikubwa sana cha kufikiri na kutatua matatizo yanayotukabiri.

Kwa waliopo vyuoni, GPA nzuri ni ya muhimu kazini na katika maisha kwa ujumla hasa aina ya ujuzi unaoupata yafaa sana ukawa tayari kuupata kwa bidii na nguvu zako zote. Si vyema kukata tama mapema katika kutafuta mafanikio kielimu kwani “hata wao walianza kama sisi” nasi tunayaweza mambo yote katika Yeye atutiaye nguvu.

Uvivu ni kizuizi kikuu cha mafanikio ya elimu kwa mwanafunzi, hata Mungu hapendi watu wavivu na “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi (kusoma), basi na asile chakula (asifauru mitihani yake)” [1 Thesalonike 3:10] naam apandacho mtu ndicho avunacho.

Kwa mantiki hiyo, kufanikiwa au kutofanikiwa kwa mwanafunzi yeyote hutegemea sana namna ya kujipanga na kukabiliana na changamoto zilizoko katika elimu. Si rahisi sana kufikia viwango vya juu vya kupata elimu rasmi (formal education) kama hazijalipwa gharama za kutosha katika upatikanaji wa elimu.

TOFAUTI ILIYOPO KATI YA ELIMU NA MASOMO YA DARASANI
Kama ilivyoelezwa hapo awali kuwa Elimu ni tendo au uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa kimaumbile wa mtu binafsi uzoefu huu unaopatikana kwa njia mbalimbali na kwa gharama kubwa huifadhiwa katika akili ya mwanadamu kwa kipindi kirefu hasa ukizingatia kuwa thamani ya elimu iko juu sana nyakati hizi ukulinganisha na  vitu vingine.

Masomo hasa yale ya darasani ni mfumo uliochaguliwa kuelezea aina furani ya elimu ili kurahisisha upatikanaji wake. Masomo ni sehemu tu ya elimu na wala sio elimu yenyewe, kwa mfano; Elimu ya viumbe hai inaelezewa kwa somo la biolojia wakati Elimu ya mambo ya kale huelezewa kwa somo la Historia n.k

Ni muhimu kama msomi mtarajiwa wa kizazi hiki na kijacho kuwa makini sana na aina ya elimu unayoitaka maishani, kwani elimu ni uzima wako wa sasa na wa baadae kwa kutegemeana na aina ya ujuzi na namna ulivyopatikana huo ujuzi. Akili ambazo Mungu amemkirimia kila mtu ni za hadhi ya juu sana na zipo ili kutufikisha mahali tunatakiwa kufika.

Hata hivyo maisha ni zaidi ya kufauru masomo ya darasani kwani ujuzi wa kilimo, biashara, mazingira na aina nyingine za elimu humwezesha mtu kufanikiwa kimaisha.


Jifunze nasi, itaendelea………………………………….